Mnyukano CCM balaa



HARAKATI za baadhi ya vigogo na wapambe wao kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na jumuiya zake, zimeanza kukitisha chama hicho.
Tanzania Daima limedokezwa kuwa Kamati Kuu (CC) ya chama hicho iliyokutana Ijumaa iliyopita chini ya uenyekiti wa Rais Jakaya Kikwete, imekubaliana kuyafyeka majina yote ya wagombea watakaobainika kushiriki kwenye vitendo vya rushwa na wenye dosari mbalimbali.
Akizungumza juzi jijini Dar es Salaam, Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC), Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye Nape alisema kuwa CC ilipokea taarifa ya maendeleo ya uchaguzi ndani ya chama na kuridhishwa na uchaguzi huo na kuagiza kila kikao husika kihakikishe haki inatendeka hasa katika uchujaji wa majina ya wagombea.
“CC imeagiza kuendelea kukemea vitendo vya rushwa kwenye chaguzi zetu. Na kuhakikisha kila anayebainika kujihusisha na vitendo hivyo au mawakala wao hatua kali za kisheria zitachukuliwa,”alisema.
Aidha, CC pia inadaiwa kukubaliana kutofanya uchakachuaji wa majina ya wagombea wanaoonekana kukubalika zaidi katika jamii kama ilivyotokea kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Inadaiwa hoja hiyo iliungwa mkono na wajumbe wengi ambao walieleza hofu yao kuwa endapo uchakachuaji huo utafanyika, kuna hatari ya kupoteza wanachama muhimu, hivyo kujiweka katika hatari ya kushindwa kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Mmoja wa wajumbe waliohudhuria mkutano huo, alisema michakato ya uchaguzi inayoendelea hivi sasa kwenye chama hicho na jumuiya zake, kwa kiasi kikubwa imetawaliwa na makundi yanayokinzana ndani ya chama hicho.
Alidai kuwa, tishio kubwa linalokikabili chama hicho ni kuzika tofauti za makundi mawili hasimu ndani ya CCM yanayodaiwa kuongozwa na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Alidokeza kuwa makundi hayo yameshaanza rafu za kuandaa safu za kufanikisha ushindi ndani ya chama ambazo pia zitawasaidia kupambana na wapinzani kwenye uchaguzi mkuu.
Kada mwingine alidai chaguzi za chama zinazotarajia kufanyika baadae mwaka huu, zinaweza kutoa taswira ya kufa au kuimarika kwa chama hicho iwapo hila, chuki na fitina zitatawala.
Alisema chaguzi hizo zinaweza kuzalisha makundi mabaya zaidi kuliko yale ya mwaka 2005 ambapo kundi la wanamtandao lililokuwa likimpigia debe Rais Kikwete lilidaiwa kuendesha siasa chafu dhidi ya wapinzani wao.
Miongoni mwa wapinzani walioshughulikiwa na wanamtandao ni Fredrick Sumaye, John Malecela na Salim Ahmed Salim walionekana kutoa upinzani mkali kwa Rais Kikwete.
Hata hivyo, baada ya CCM kumpitisha Kikwete, inadaiwa makundi hasimu yaliendelea kukinzana, hivyo kusababisha chama na serikali kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.
Mbali na hayo CC imepinga kauli za Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Membe na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama, Lowassa juu ya mvutano baina ya Tanzania na Malawi.
Kwa mujibu wa chanzo cha habari kutoka ndani ya kikao hicho, wajumbe walipinga hatua zozote za maandalizi ya kuingia vitani na Malawi juu ya kugombea mipaka ya Ziwa Nyasa.
Kilidokeza kuwa, wajumbe wengi waliunga mkono kauli ya Rais Kikwete, kuwa Tanzania haina sababu ya kuingia vitani na nchi hiyo jirani bali wataalamu wa nchi zote mbili wapewe fursa ya kufanya mazungumzo.
Katika hilo, Nape alisema kuwa CC ilipokea taarifa ya mgogoro huo na kuridhika na hatua zilizochukuliwa kuutatua kwa njia ya amani na hivyo kuwatahadharisha wanasiasa na vyombo vya habari vinavyochochea vita na uhasama kati ya nchini hizo kuacha mara moja na kuiachia diplomasia ichukue mkondo wake.
Mwakyembe, Kagasheki wasifiwa
Katika hatua nyingine CC, imeeleza kuridhishwa na utendaji wa mawaziri, Dk. Harrison Mwakyembe wa Ujenzi, Balozi Khamis Kagasheki wa Maliasili na Utalii na Dk. Abdallah Kigoda wa Viwanda na Biashara katika kuwachukulia hatua wakuu wa mashirika ya umma waliojihusisha na ubadhirifu.
Bila kuwataja kwa majina, Nape alisema kuwa CC ilipokea taarifa ya maendeleo ya utekelezaji wa maagizo yake juu ya kushughulikia mapungufu yaliyooneshwa kwenye taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kamati mbalimbali za Bunge.
“CC imeipongeza serikali kwa hatua zilizoanza kuchukuliwa dhidi ya mapungufu hayo, hasa hatua dhidi ya wakuu mbalimbali wa mashirika kadhaa ya umma, kama vile Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO), Shirika la Viwango (TBS), Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Shirika la Ndege Tanzania (ATC) na Wizara ya Maliasili na Utalii,” alisema.
Hata hivyo, licha ya kutotajwa kwa majina, mawaziri hao watatu wameanza kazi kwa vitendo ikiwa ni kuwasimamisha kazi baadhi ya vigogo kwenye wizara zao waliokuwa wakituhumiwa kujihusisha na ufisadi.
Dk. Mwakyembe ameanza kwa kumsimamisha kazi aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa ATC, Paul Chizi na wakurugenzi wanne kutokana na ukiukwaji wa sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma. Na wiki aliyopita amemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu TPA, Ephraim Mgawe na viongozi wengine watatu ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali za ufisadi zinazowakabili.
Waziri Kigoda yeye alianza kazi kwa kumsimamisha aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Charles Ekelege ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za ufisadi zilizokuwa zikimkabili.
Agosti 13 mwaka huu, Waziri Kagasheki, alitangaza kuwatimua kazi vigogo watatu wa wizara yake akiwamo Mkurugenzi wa Wanyamapori, baada ya kubainika kuhusika katika kashfa ya utoroshaji wanyamapori hai kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwenda nje.
Vile vile wiki aliyopita, alitangaza kubadili utaratibu za kuwapata wajumbe wa bodi zilizoko chini ya wizara ambapo kuanzia sasa watapatikana kwa njia ya ushindani badala ya kuteuliwa moja kwa moja na waziri.
Nape aliongeza kuwa, itakumbukwa kuwa CC iliagiza pamoja na viongozi wa kisiasa kuchukuliwa hatua kwa mapungufu yale, ipo haja ya kuwachukulia hatua watendaji wakuu wa mashirika yaliyohusishwa na ubadhirifu mbalimbali.
“Kamati Kuu inawapongeza mawaziri husika na watendaji wote wa serikali walioanza kutekeleza agizo hili kwani mwisho wa siku maisha bora kwa kila Mtanzania yatawezekana,” alisema.

Comments

Popular posts from this blog