Kitaeleweka: Liverpool, Man City zatunishiana misuli

Kocha wa Man City Roberto Mancini
ONDON, ENGLAND
LIGI Kuu England imeanza tangu wiki iliyopita, lakini utamu halisi utaanza kesho Jumapili wakati Liverpool na Manchester City zitakapokwaana katika Uwanja wa Anfield.

Kila kikosi kitaingia uwanjani kusaka ushindi, Manchester City inataka kuendeleza ubabe baada ya kuinyoa Southampton mabao 3-2 wikiendi iliyopita ikiwa ni ushindi wa tano katika mechi tano za karibuni.

Kwa upande wake, Liverpool haiwezi kukubali kuwa wateja kwa mara nyingine kufuatia kufungwa mabao 3-0 na West Brom wiki iliyopita.

Manchester City inakwenda katika mechi hiyo ikiwa na historia nzuri katika siku za karibuni, lakini timu hizo zilipokutana katika mechi tano za nyuma, Liverpool ilipata ushindi mara mbili, Manchester City mara moja na walitoka sare katika mechi mbili.

Liverpool haitakuwa na beki Daniel Agger, ambaye amefungiwa mechi moja na Manchester City itawakosa wachezaji watatu ambao wameumia.

Mshambuliaji, Sergio Aguero, kiungo Gareth Barry na beki Micah Richards wote ni majeruhi.

Ukiachilia mbali mechi hiyo, Manchester United ambayo Jumatatu wiki hii ilikaribishwa katika ligi kwa kichapo cha bao 1-0 kutoka Everton, huenda ikazinduka wakati itakapokutana na Fulham leo Jumamosi.

Manchester United imenasa nyota wazuri kama Shinji Kagawa na Robin van Persie, lakini ilishindwa kutamba mbele ya Everton.

Baada ya mechi hiyo kocha, Alex Ferguson, alikiri kufanya makosa kutomwanzisha Van Persie katika kikosi cha kwanza na badala yake nyota huyo aliingia uwanjani dakika 22 kabla ya kipenga cha mwisho

Hata hivyo wapinzani wao Fulham wapo katika hali nzuri baada ya kuisambaratisha Norwich City mabao 5-0 katika mechi ya fungua dimba.

Nayo Chelsea itakuwa na wakati mgumu itakapoivaa Newcastle United leo Jumamosi. Katika mechi ya awali Chelsea iliifunga Wigan Athletics mabao 2-0 na katikati ya wiki hii iliinyuka Reading mabao 4-2.

Hata hivyo Newcastle United ambayo ilimaliza msimu uliopita katika nafasi ya tano juu ya Chelsea, ilianza ligi kwa kutoa kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya Tottenham.

Nayo Arsenal ambayo ilianza ligi kwa suluhu dhidi ya Sunderland, itataka kuzinduka wakati itakapokuwa ugenini kupambana na Stoke City kesho Jumapili wakati Tottenham itakwaaana na West Brom leo Jumamosi.

Comments

Popular posts from this blog